Popular Posts

Wednesday, March 3, 2010

Wabunge wamjia juu Zitto Kabwe

Na Deogratius Temba

SIKU mbili baada ya Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kaskazini (Chadema) Zitto Kabwe, kutangaza kuteua kamati maalum ya wasomi kufanya utafiti wa jimbo gani agombee, wabunge wanaoshikilia majimbo aliyoyataja kwa sasa wamemtaka kusitisha nia yake hiyo kwani atashindwa vibaya.

Pia wamemtaka kuendelea kuwasaidia wananchi wa Kigoma Kaskazini kwani majimbo mengine anayaotaka kwenda yana wenyewe na kugombea huko atahitaji kujipanga zaidi.

Zitto aliunda kamati maalum aliyoiita ni ya wataalamu na wasomi kufanya utafiti katika majimbo ya Kigoma Kaskazini ukiondoa kata ya Mwandiga, ambayo imependekezwa kukatwa na kupelekwa Jimbo la Kigoma Mjini na hivyo kuondoa zaidi ya wapiga kura 15, 000 kutoka jimbo la Kigoma Kaskazini la sasa.

Mbali na Kigoma Kaskazini, Zitto ameiotaka kamati yake hiyo kufanya uchunguzi katika majimbo ya Kigoma Mjini, Kahama, Kinondoni na Geita.

Akizungumza kwa nyakati tofauti na Tanzania Daima jana wabunge hao walionyesha kushtushwa na kauli hiyo ya Zitto huku wakihoji sababu ya yeye kuacha jimbo lake la uchaguzi analoliwakilisha kwa sasa kuamua kuingia katika majimbo mengine.

Mbunge wa Jimbo la Kahama James Lembeli (CCM), alisema Zitto akigombea Ubunge katika jimbo la Kahama, atashindwa kwa kiasi kikubwa kwani wananchi wa Kahama wapo makini katika kuangalia mtu wa kuwatumikia.

“Siamini kama maneno hayo yametolewa na Zitto menyewe na amefikiria nini hadi anatamani majimbo mengine, kama ni kweli basi anatatizo. Kigoma kuna tatizo gani? ni kwanini anakimbia huko, kinachomfukuza Kigoma ndicho anachokifuata Kahama nina muonya asijaribu kuja ataaibika vibaya,” alisema Lembeli na kuongeza:

“ Mimi nipo tayari, nitapambana naye popote atakapokwenda, kwani kwa historia yake ya siku za karibuni ni mtu wa kutumika sasa Kahama hatupo tayari,”

Lembeli alisema kuwa sii kweli kuwa wazee wa Kahama walimwomba Zitto kugombea katika jimbo hilo kama alivyosema kwani kinachomdanganya ni jinamizi lake la Buzwagi, ambao ilikuwa ni hoja yake na Zitto akaipora na kuiwasilisha Bungeni.

“Hata hile hoja ya Buizwagi Bungeni mwaka 2007, ambayo ilimpa umaarufu ili kuwa yakwangu, yeye akanipora, akaibuka nayo kwani mimi ndiye niliyehoji Bunge juu ya mkataba wa Buzwagi wakati sijajibiwa yeye akaiwasilisha kama hoja binafsi, lakini wananchi wa Kahama hawataki kurudi huko, na hawataki watu wa aina ya Zitto,’alisema

Lembeli alitamba kuwa yeye ni Komandoo na yupo radhi hata kama Jimbo la Kahama litagawanywa kuwa mawili, atapambana na Zitto katika jimbo moja wapo atakalogombea ili ahakikishe anashindwa na kuaibika na ana wasiwasi kuwa ametumwa kugombea katika jimbo hilo.

Lembeli aliendelea kuhoji kwamba ni kitu gani mbacho Zitto amewafanyia wananchi wa Kigoma Kaskazini ambacho wananchi wa Kahama hawana? na kama hajaweza kuwasaidia wananchi wake atawezaje wa Kahama?.

Naye Mbunge wa jimbo la Kindondoni, Idd Azzan, alipoulizwa alisema kwasababu bado yeye hajateuliwa kugombea nafasi ya Ubunge katika jimbo hilo kwa sasa anasita kusema kitu ila kama atateuliwa atapambana na Zitto.

Unajua bado kuna mchakato ndani ya chama sijui kama mimi ndiye nitakayegombea kipindi kingine, na bado sijatangaza kugombea lakini kama nitagombea nitapambana naye,” alisema Azzan kwa ufupi.

Peter Serukamba, wa Kigoma Mjini, alisema, kauli ya Zitto ya kuwa ametuma watu kufanya utafiti katika jimbo hilo, ni haki ya msingi ya Mbunge huyo, na hawezi kumshauri chochote zaidi ya kusubiri wakati ufike.

“ Ni haki yake ya msingi na ya kikatiba kufanya hivyo, lakini siwezi kumshauri ila kama ni kweli anataka kuja itabidi ajipange,”alisema Serukamba.

Juzi Zitto alinukuliwa katika taarifa yake kwa vyombo vya habari kuwa ameunda kamati ya uchunguzi (Exploratory Committee) ya watu watatu kwa ajili ya kufanya utafiti wa kina juu ya jimbo gani nigombee Ubunge katika uchaguzi Mkuu wa Mwezi Oktoba mwaka huu.
mwisho

No comments:

Post a Comment