Popular Posts

Friday, March 5, 2010

Kwaresma iguse maisha yetu, tunapoingia kwenye uchaguzi

Na Deogratius Temba

KWARESMA ni kipindi cha mfungo kwa waumini Wakatoliki. Mfungo huu ni wa siku hamsini. Kipindi hiki kinaanza na ibada ya kupakwa majivu kwenye paji la uso (siku ya Jumatano ya Majivu) ikiwa ishara ya kuanza toba. Kujikubali kwamba tu wakosefu na pia kujutia makosa yetu tunayotenda kinyume na mapenzi ya Mungu.

Kipindi cha Kwaresma kinatuandaa waumini Wakatoliki kwa ajili ya Sikukuu ya Pasaka yaani ufufuko wa Yesu Kristo. Ufufuko ndio msingi mama wa imani yetu sisi Wakatoliki; “…na kama Kristo hakufufuka, basi mahubiri yetu hayana maana na imani yetu haina maana…” (1 Wakaritho15:14).

Kipindi cha Kwaresma kinadai mambo makuu matatu: Kwanza, kufunga yaani kubadili aina na kiasi cha chakula ambacho mtu huwa anakula kila siku, kiasi kipungue na aina pia ya chakula. Kama wewe umezoea kula milo mizito yenye kila aina ya mahanjumati basi Kwaresma badilisha na ule kawaida kabisa.

Kufunga hakuishii tu katika kufunga chakula bali kuzuia mianya yote inayomfanya mtu atende dhambi. Hili ndilo jambo la kuzingatia. Kama tunavyosoma katika Kituo cha 14 cha njia ya msalaba kinachosema kwamba; “Pamoja nawe kaburini, zika dhambi na ubaya wa moyo, Yesu tuwe Wakristo kweli. Twakupa, twakupa sasa mapendo.”

Ni kipindi cha kujinyima na kujikatalia: Pili, kufanya matendo ya huruma au kutoa sadaka, yaani kile ambacho mtu anajinyima basi akipeleke kwa wenye shida.

Tatu, kuongeza muda wa kusali hasa kwa kusoma Neno la Mungu, yote haya matatu yanaelezwa vizuri sana katika kitabu cha Nabii Yoel 2:12-18.

Kwa Wakatoliki, tendo hili la Kwaresma huwa linajionyesha kwa kufuata njia ya msalaba ambayo huwa inafanyika siku ya Ijumaa na sehemu nyingine siku ya Jumanne. Bila ya kujali ni siku ngapi za njia ya msalaba mtu anahudhuria.

Kinachozingatiwa zaidi ni kuona kuwa vile vituo vyote kumi na nne vya njia ya msalaba vina maana katika maisha ya ufuasi wa Yesu Kristo au tunahudhuria ibada kwa kutekeleza wajibu wa kuonekana kwamba tunapitia vituo vyote kumi na nne kwa masikitiko ya usoni kumbe moyoni ni mkavu kabisa.

Vituo vya njia ya msalaba havitukumbushi tu machungu na magumu aliyopitia Yesu bali kikubwa zaidi ni sisi waumini tunakumbushwa kujitoa na kuacha mapenzi na makusudi ya mtu yanayomjengea ubinafsi, ili aweze kumfuata yeye aliyejitoa kwa ajili yetu maskini kwa matajiri.

Yesu hadai kwamba mwumini lazima apate adha na mateso ya kimwili, lakini anataka kila mfuasi wake awe tayari kutimiza mapenzi ya Mungu ambayo kwayo yanadai zaidi kutimiza na kuishi amri ya mapendo ambayo imeonekana kupitia kwa Yesu Kristo.

Ushiriki wa njia ya msalaba haumfanyi mtu kumtafuta Mungu au kuwa karibu na Mungu tu, bali ushiriki wa ibada ya njia ya msalaba unatufanya na kutulazimu tukuze mapendo kwa ndugu zetu kwa kukwepa na kuogopa kuwafanyia mabaya.

Neno haki linakuza na kudumisha upendo, kinyume cha hapo kunakuwa na magomvi, matabaka yasiyo ya lazima, uonevu, unyanyasaji, udhalilishwaji na ubadhirifu wa kila namna na ndipo ufisadi unajikita kwa sababu haki imepindishwa na kutekwa na wenye nguvu.

Haki katika safu hii naiweka katika maana mbili; kwa upande mmoja haki ina maana ya usawa, uadilifu au uwajibikaji kuhusu sheria ya mambo ya kawaida ya jumuiya ya mwanadamu. Hii tunaweza inaitwa ‘justice’.

Sheria ya kutambua haki hii imeandikwa kwenye moyo wa kila mwanadamu na inaitwa dhamira; “…Mwenendo wao unaonyesha kwamba matakwa ya sheria yameandikwa mioyoni mwao. Dhamira zao zinashuhudia pia jambo hili, maana fikra zao mara nyingine huwashitaki, na mara nyingine huwatetea…” (Warumi 2:15).

Sheria kama hizi hazijaandikwa kwenye vitabu bali ziko katika moyo wa mtu, mbali na kuwa haiko katika vitabu lakini bado inambana mwanadamu ajue haki ni nini na apange kanuni ili kuendesha haki katika jamii. Utambuzi wa haki hii haikuandikwa lakini bado unamwezesha mwanadamu afahamu yaliyo sawa au yanakwenda kinyume na Mungu.

Kipindi hiki cha Kwaresma kinatubana zaidi kuhakikisha tunadumisha upendo kwa kutenda haki katika taasisi zote za kiserikali na dini, kwani sote twahesabika kuwa tu wadhambi twaweza tukawahadaa wanadamu wenzetu lakini Mungu bado anaona mioyo yetu kama Nabii Amosi anavyotuambia; “…maana mimi najua wingi wa makosa yenu na ukubwa wa dhambi zenu; ninyi mwawatesa watu wema, mnapokea rushwa na kuzuia fukara wasipate haki mahakamani.” (Amosi 5: 12).

Ujumbe wa Kwaresma wa maaskofu wakatoliki kwa waumini mwaka huu umeeleza mambo mengi ya msingi yanayogusa maisha yetu hasa katika kipindi hiki taifa linapoelekea katika uchaguzi Mkuu na ukiongozwa na dhamira kuu isemayo “Ninyi ni Chumvi ya Dunia…” (Mt 5:13).

“Kama tunavyofahamu, nchi yetu iko katika mchakato wa uchaguzi mkuu, utakaofanyika Oktoba 2010. Uchaguzi huo utatupatia viongozi wapya: madiwani, wabunge na rais wa nchi yetu.

“Uchaguzi huo ni tukio la kijamii na vile vile ni tukio la kisiasa. Ni tukio ambalo Wakristo wote wanapaswa kushiriki kama wajibu wao. Historia yatwambia kwamba, ushiriki wa Wakristo katika mambo ya ulimwengu umekuwa wa namna tofauti katika kipindi cha zaidi ya miaka 2000,”

“Tunaomba sana na kuwasihi wale wote wanaogombea katika nafasi hizo za uongozi wafikiri na kutafakari kwa makini ni kitu gani kimewasukuma ili kuchukua hatua hiyo? Wanataka kwa moyo wao wote kuwatumikia Watanzania ili kila mtu katika jamii yetu apate hadhi yake ya kiutu ambayo ni stahili yake?” ulihoji waraka huo.

Maaskofu wamewataka wagombea wote kujiuliza kama kweli wana nia ya dhati ya kuwasaidia Watanzania ili kila mtu apatiwe mahitaji msingi ya kumwezesha kuishi maisha yanayomstahili mwanadamu, pamoja na kuwa tayari kuzifanya rasilimali za nchi yetu kuwa kwa ajili ya manufaa ya wote.

Kwa muda wa takaribani mwaka mmoja na nusu, tumekuwa pamoja katika safu hii, tumejadili mengi na kufundishana, bila shaka kila mmoja alijifunza nikiwepo mimi binafsi ambaye nilipata mengi kutoka kwa wasomaji wangu. Ninawashukuru sana wasomaji kwa ushauri. Nimejisiki niko na watanzania wengi karibu kupitia tafakuri hii. nawapenda sana! Mungu awabariki.

Nimeamua leo, tufanye tafakuri ya pamoja ya mwisho ya kiroho zaidi ili tuagane, ninatarajia kuanzisha safu nyingine ya kisiasa siku za katikati ya wiki, nimeisimamisha safu ya Jumapili kutokana na kubanwa na masomo.
Tutaendelea kuwasiliana kwa mawazo na hata kuchangia zaidi katika blog yangu.
deojkt@yahoo.com
www.deotemba.blogspot.com
0784/ 715 686575

12 comments:

  1. ASANTE SANA NDUGU DEOTEMBA KWA KWELI UMEFAFANUA VIZURI KIASI KWAMBA KILA MTU ANAELEWA MAANA YA KWARESIMA NA KUFUNGA. NATUMAINI WENGI HAWAELEWI MAANA YA KUFUNGA NA PIA KWARESIMA HAWAELEWI NI NINI CHA KUFANYA KUTOKANA NA KUSIKIA WENGINE WAKIDAI KUWA KWA NINI UJINYIME UJITESE. MUNGU HAPENDI MTU ANAYEJITESA. WENGINE WANASEMA KWA NINI KWARESIMA WATU WAFUNGE. HAWAONI UMUHIMU WOWOTE KWA KUWA HAWAELEWI. NAOMBA UENDELEE KUANDIKA MAMBO MENGI ILI WATAKAOJISOMEA WAPATE FAIDA YA KIROHO.

    ReplyDelete
  2. Nakushukuru sana kwa tafakari nzuri sana ya maana halisi ya Kwaresma na pia ningelipenda kuongezea kwamba Kwaresma iwe ni chachu na chanzo cha mabadiliko ya kiroho na si kwamba baada ya Paska basi mtu anasahau yote na kuifanya roho ife ganzi kwa kurudia uovu!!!
    Kwa maombi ya kweli,yote yanawezekana maana huruma ya MUNGU kwetu ni ya kipekee haijalishi ulikua mdhambi kiasi gani lakini toba ya dhati ndiyo nguzo imara ya mahusiano mazuri na MUNGU wetu!!!
    Tumsifu YESU KRISTO....

    ReplyDelete
  3. Kazi nzuri sana. Mwanzo ni mgumu lakini HAKIKA utafika. Maltin Luther alisema "kama huwezi kuruka,kimbia. Na kama huwezi kukimbia basi tembea. Na kama huwezi kutembea basi haidhuru tambaa..ili mradi uondoke pale ulipo na kusogea mbele.Muwe na Kwaresma ya BARAKA. mwana-dikala.

    ReplyDelete
  4. Napingana kidogo kwa kusema Kwaresma ni mfungo wa siku hamisini, ukweli ni kwamba ni mfungo wa siku 40 ukianzia na Jumatano ya majivu

    ReplyDelete
  5. When is the right time to unfast?

    ReplyDelete