Popular Posts

Wednesday, May 26, 2010

MV. Liemba Meli kubwa, yenye umri mkubwa kuliko zote nchini

*Ilizamishwa ziwani na wakaoloni baadaye ikafufuka
*Ina Umri wa miaka 98, mwaka 2013 itavunja rekodi ya dunia
Na Deogratius Temba
MV Liemba ni meli ya Kitanzania inayohudumia pwani za Ziwa Tanganyika. Ni chombo cha usafiri wa majini chenye umri mkubwa kuliko kingine chochote nchini na kipo tangu mwaka 1914.
Meli hii kama zilivyo meli ningine inasukumwa na injini ya diseli na ina urefu wake ni mita 67, upana mita 10 na uzito wa tani 1500.
MV. Liemba, ina uwezo wa kubeba abiria 600, pamoja na mzigo tani 200 kati ya bandari ya Ziwa Tanganyika upande wa Tanzania inaegeshwa katika bandari ya Kigoma, Zambia bandari ya Mpulungu, Kongo- Kalemie, na Burundi ni Bujumbura.
Mv. Liemba ilivyoanza kutengenezwa
Mv. Liemba ilitengenezwa nchini Ujerumani mwaka 1913 ikiwa ikiitwa kwa "Graf von Goetzen" kwenye kiwanda cha meli cha Meyer huko Papenburg, ikikusudiwa kwa huduma ya mizigo na abiria kwenye Ziwa Tanganyika.
Baada ya kukamilika meli iliondolewa vipande vyote hadi ribiti zake 160,000 vilifungwa katika masanduku 5,000 na kubebwa kwa meli kubwa hadi Dar es salaam. Ilifika mwaka 1914 muda kidogo kabla ya mwanzo wa vita kuu ya kwanza ya dunia.
Mafundi watatu kutoka Papenburg waliongozana na masanduku ya meli kwa njia ya reli hadi Kigoma. Hapa sehemu zote za meli ziliunganishwa tena kwa msaada wa wafanyakazi Waafrika 250 na Wahindi 20.
Februari 5, 1915 "Graf von Goetzen" iliingizwa katika maji ya Ziwa Tanganyika, katika bandari ya Kigoma.
MV. Liemba wakati wa Vita Kuu ya Kwanza
Kwa sababu za vita meli iliongezwa mizinga kutoka manowari SMS Koenigsberg ikawa meli kubwa yenye silaha ziwani. Mwaka 1916 Waingereza na Wabelgiji walishambulia koloni ya Kijerumani kwa nguvu wakafaulu kuzunguka ziwa kwa njia ya nchi kavu na kukata njia ya reli kutoka Kigoma kwenda Tabora. Hapa Wajerumani waliamua kujiondoa ziwani na kuungana na jeshi lao ndani ya nchi.
Mafundi Wajerumani kutoka Papenburg waliopaswa kubaki Afrika kutokana na vita walipewa amri na maadui zao kuzamisha meli hiyo ziwani. Mafundi hao kwa hiari yao waliamua kutoharibu meli lakini kuizamisha kwa njia itakayowezesha kufufuka kwake.
Hivyo walipaka mashine zote mafuta mazito wakajaza vyumba vya mizigo kwa mchanga na kuzamisha meli polepole. Tukio hili lilifanyika Julai 26, 1916 kwenye sehemu ya ziwa isiyo na kina kubwa karibu na mdomo wa mto Malagarasi.
Kufufuliwa kwa MV Liemba
Hivyo waliwawezesha Waingereza washindi wa vita kufufusha meli mwaka 1924 na kuitumia tena, kilichoshangaza ni kwamba mafundi walipoijaribu Meli wakikuta mashine zote zikifanya kazi baada ya kusafishwa.
Meli ilipewa jina MV Liemba kutokana jina la kale la Kifipa (asili ya Sumbawanga) likimaanisha ‘ kwa ajili ya ziwa’, ikaendelea kufanya huduma ziwani hadi leo.
Tangu 1961 ilikuwa meli ya Jamhuri ya Tanganyika na baadaye Tanzania.
Matengenezo ya MV.Liemba
Injini ya mvuke ya awali imebadilishwa mara kadhaa sasa ni injini ya diseli. Hadi leo imeendelea kutoa huduma bila ajali kutokana na uimara wake.
Mv Liemba inahitaji kufanyiwa matengenezo makubwa ili kuirejesha katika hali bora ya kuendelea kusafirisha abiria na mizigo katika ziwa Tanganyika.
Meneja wa wakala wa huduma za meli mkoa Kigoma Projest Kaija amesema meli hiyo imezeeka sana na inatakiwa kusimama kufanya kazi katika kipindi kifupi kijacho.
Balozi wa Ujerumani nchini Dk.Guido Hertz, alipoimbelea meli hiyo kuona namna gani Ujerumani inavyoweza kusaidia katika ukarabati huo, alisema kuwa mwaka 2013 meli hiyo itakuwa inatimiza miaka 100 tangu ianze kufanya kazi na kuifanya kuwa meli ya abiria iliyofanya kazi kwa muda mrefu duniani.
Nahodha wa meli hiyo Titus Benjamen anasema kuwa kwa sasa hakuna njia mbadala ya kuweza kuwahudumia abiria na mizigo wanaosafiri katika mwambao wa ziwa Tanganyika ambao wanategemea meli hiyo kwa safari zao mbalimbali.
Balozi Hertz, anasema kuwa wazo la kuifanyia ukarabati meli hiyo ni zuri na kwamba ataishawishi serikali ya nchi yake kuona namna gani inasaidia katika kutoa fedha za kufanikisha jambo hilo.
Katika ushawishi huo anakusudia kuiomba serikali ya Ujerumani kununua meli nyingine mpya ya abiria kwa ajilia ya kuhudumia wananchi waliokuwa wakihudumiwa na meli hiyo ili meli hiyo iwe inatumika kwa shughuli za utalii.
Mchango wa MV. Liemba kwa uchumi wa wananchi
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Daniel Ole Njolay, anasema inasikitisha kuona kwamba wananchi wa Rukwa wanashindwa kufanya biashara kubwa na jirani zao wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC), wanaopakana nao kwa sababu ya ukosefu wa maboti au vivuko.
Anasema kuwa meli ya Mv. Liemba haiwanufaishi wananchi hao kiuchumi kutokana na kutokidhi mahitaji ya safari za meli katika ziwa hilo na mkoa wake kutokuwa na Bandari.
Anabainisha bila kutafuna maneno kuwa, tatizo hilo linasababishwa na fukwe za upande wa Rukwa katika ziwa hilo hilo la Tanganyika kutokuwa na bandari nzuri.
Meli ya Liemba kwa mfano hufanya safari zake kati ya bandari ya Kigoma na Mpulungu, Zambia na kunegesha biashara mbalimbali kati ya watu wa bandari hizo, biashara ambayo inakosekana Rukwa kutofikiwa kwa meli hiyo.
Anasema kama kungekuwa na miundombinu ya uhakika, wana Rukwa wangeweza kufanya biashara nzuri na Wakongo kwa kuwauzia simenti, Sukari, chumvi na hata nafaka.
“Kwa kweli tungekuwa na meli kubwa kwa mfano, mkoa huu ungekuwa na uchumi mzuri, lakini kitu kama hicho hakipo,” anasema.
Mwaka jana yeye na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, walifanya mkutano wa ujirani mwema na gavana wa Katanga ambapo walizungumzia mambo mengi muhimu kuhusu pande zote.
Njoolay anasema kuwa wao kwa upande wao waliona kuna umuhimu wa wafanyabiashara nchini na wawekezaji kwa ujumla kujikita katika shughuli za uvuvi na biashara nyingine kando ya ziwa Tanganyika.
Anasema miondombinu ni tatizo kubwa mkoani Rukwa. Barabara ni za vumbi hivyo hupitika kwa shida wakati wa masika na hiyo inafanya shughuli nyingi za uchumi kukwama.
mwisho

No comments:

Post a Comment