Popular Posts

Wednesday, May 26, 2010

Miaka 14 ya ajali ya MV Bukoba: Tumejifunza nini?

*Ni ajali iliyoweka historia kwa kuua
*Bado usalama wa ziwani haujaimarika
Na Deogratius Temba
MEI 21, mwaka huu taifa limetimiza miaka 14 tangu ilipotokea ajali mbaya na ya kusikitisha iliyosababishwa na kuzama kwa meli ya MV Bukoba.
Ajali hiyo ilitangazwa kuwa ni msiba wa kitaifa na kufuatia rais wa awamu ya tatu Benjamin Mkapa, kutangaza siku tatu za maombolezo na bendera kupepea nusu mlingoti.
Tunawakumbuka ndugu zetu waliokufa katika ajali hiyo.
Kutokana na ajali hiyo, serikali imejifunza nini na imechukua hatua gani kukabiliana na majanga ya ajali zinazotokea hapa nchini, ikishirikiana na Mamlaka ya Udhibiti na Usafiri wa Vyombo vya Majini na Nchi Kavu ( SUMATRA)? Meli hiyo ambayo ilizinduliwa mwaka 1979 na Rais wa kwanza wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Nyerere, ilidumu kwa miaka 17 tu, na kupinduka ikiwa katika safari zake za kawaida, ikitokea katika bandari ya Bukoba kupitia Kemondo.
Meli hiyo ya MV Bukoba ilipinduka na kuzama ndani ya Ziwa Victoria Siku ya Jumanne alfajiri Mei 21, 1996. Kuzama kwa meli hiyo kulisababisha watu zaidi ya 800 kupoteza maisha baada ya kufa maji.
MV Bukoba ilizama ikiwa imebakisha umbali wa maili moja na nusu ili iweze kutia nanga katika bandari ya Mwanza Kaskazini, hali ambayo ilikwishawapa abiria matumaini ya kufika salama kwa abiria waliokuwa ndani ya meli hiyo.
Ilikuwa tayari iko jirani kabisa na ufukwe wa Shule ya Sekondari Bwiru, ambako sasa kumejengwa mnara wa kumbukumbu ya wahanga wa ajali hiyo mbaya kuwahi kutokea katika Ziwa Victoria na katika historia ya Tanzania tangu kupatikana kwa uhuru.
Ukosefu wa vifaa vya kuokolea majini ulikuwa ni chanzo cha kuongezeka kwa vifo vya abiria, waokoaji wa ajali hiyo walisubiriwa kufika nchini kutokea Afrika ya Kusini, ambao waliweza kuogelea na kuokoa baadhi ya maiti chache zilizokuwa zimezama umbali wa mita 25 chini ya maji.
Ajali hiyo imebaki kuwa kumbukumbu mbaya kwa wakazi wa Kanda ya Ziwa na mikoa jirani. Kila mwaka ifikapo Mei 21 hapa Tanzania, siku hiyo hukumbukwa kwa kuomboleza vifo vya abiria waliokuwa ndani ya meli hiyo.
Katika kitabu cha SITAISAHAU MV BUKOBA kinachoelezea hali halisi ilivyokuwa ndani ya meli ya MV Bukoba kabla na baada ya ajali. Nyaisa Simango ni miongoni mwa abiria wachache tu walionusurika katika ajali hiyo. Anaelezea safari yake tangu mwanzo akitoka Dar es salaam kwa treni hadi Mwanza, na kutoka Mwanza kwenda Bukoba, na safari yake ya kurudi kutoka Bukoba na meli hiyo hadi ilipoishia kwa kupinduka na kuzama.
Simango ameeleza katika kitabu kuwa hata siku ya kwanza kuelekea Bukoba, bandarini Mwanza Meli ilikuwa imejaa kwa kiasi kikubwa.
Baadhi yao miili yao haikupatikana na kusababisha maziko yao kufanyika humo humo majini huku meli hiyo ikigeuzwa kuwa kaburi lao la pamoja.
Makaburi ya wahanga wengine yapo katika Kitongoji cha Igoma umbali wa kilometa nane kutoka katikati ya Jiji la Mwanza.
Katika ajali ya meli hiyo mali ya Kampuni ya Huduma za Meli Tanzania (MSC) iliyokuwa chini ya Shirika la Reli (TRC), hadi leo bado ni kitendawili kilichokosa mteguaji, kuhusu idadi kamili ya abiria waliokuwamo ndani ya meli hiyo.
Yapo madai kuwa ilikuwa imebeba zaidi ya abiria 1,200 na mizigo iliyokuwemo ikiwa inakadiriwa kuwa zaidi ya tani 200. Inadaiwa kuwa watu 1,000 walipoteza maisha huku abiria 112 tu wakinusurika katika ajali hiyo.
Wakati tukielezwa kuwa meli ilikuwa na uwezo wa kubeba abiria 430, kwenye daraja la kwanza na la pili orodha ya abiria ilikuwa 443, wakati daraja la tatu ambazo kwa kawaida hubeba abiria wengi zaidi hakukuwepo rekodi yoyote.
Meli hiyo ambayo ilikuwa ya pili kwa ukubwa kati ya meli zinazofanya safari zake katika Ziwa Victoria, ajali yake iliacha simanzi na majonzi makubwa miongoni mwa familia nyingi ambazo ndugu zao walikuwa miongoni mwa abiria waliokuwa ndani.
Tangu kutokea kwa ajali hiyo mbaya, ukiondoa ile ya treni ya abiria iliyotokea Igandu na Msangali, baada ya treni ya mizigo kugongana na treni ya abiria mwaka 2001 na kusababisha vifo vingi vya abiria, bado serikali hajapata dawa ya kukomesha ajali ndani ya Ziwa Victoria.
Sehemu kubwa ya Tanzania inayotumia usafiri wa meli katika ziwa hilo linalozunguka nchi tatu za Kenya, Uganda na Tanzania ni Mwanza, Bukoba na Ukerewe. Hadi sasa hakuna sababu zilizokwishatolewa kuhusu chanzo cha ajali ya MV Bukoba ingawa wapo baadhi ya watu na viongozi wanaosema ilitokana na meli hiyo kujaza abiria na mizigo kupita kiasi, na kwamba ilikumbwa na dhoruba kali ziwani.
Meli hiyo ambayo ilijengwa na kampuni ya Kibelgiji, tangu kuzinduliwa kwake ilikuwa na tatizo la uwiano.
Aidha, yapo madai kuwa kabla ya safari hiyo ya mwisho kwa meli ya MV Bukoba ilikuwa mbovu, na hakuna mtu ambaye amewahi kutajwa kuiruhusu kufanya safari zake huku ikiwa mbovu, tofauti na kubebeshwa mzigo wa lawama nahodha wake, Jumanne Lume Mwiru ambaye alifunguliwa kesi na wenzake kwa kosa la uzembe, kusababisha vifo vya watu 400, kujeruhi na upotevu wa mali zisizofahamika.
Kesi hiyo iliahirishwa mara sita, baada ya kusikilizwa na hatimaye Ijumaa Novemba 29, 2002 aliyekuwa Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mwanza, aliwachilia huru washitakiwa wote wanne.
Aliwachia baada ya upande wa mashitaka kushindwa kuthibitisha mashitaka yao. Hukumu hiyo yenye kurasa 118 iliyoandikwa kwa mkono, ilisomwa kwa zaidi ya dakika 160, ikianza tangu saa sita mchana hadi saa tisa adhuhuri.
Washitakiwa wa kesi hiyo walikuwa nahodha huyo, Mkuu wa Bandari ya Kemondo, Prosper Lugumila, Mkuu wa Bandari ya Bukoba, Alfred Sambo, ambaye sasa ni marehemu na Mkaguzi wa Mamlaka ya Bandari (THA), Gilbert Mokiwa.
Tangu kutolewa kwa hukumu hiyo, hakuna mtu yeyote aliyejitokeza kueleza sababu za ajali ya meli hiyo hadi sasa.
Kutokana na ajali hiyo, serikali iliunda SUMATRA kwa ajili ya kukabiliana na matatizo ya ajali ikiwa na lengo la kufanya ukaguzi kwa vyombo vyote vya usafiri wa majini na nchi kavu.
Pamoja na kuwepo kwa chombo hicho, bado ajali zimeendelea kutokea kila kukicha, mwaka 2008 nusura yajirudie yale ya MV Bukoba, baada ya Mbunge wa Ilemela, Anthony Diallo na wenzake kunusurika kufa baada ya boti waliyokuwa wakisafiria kwenda katika mazishi ya Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Ukerewe, kuzama.
Meli ya MV Mlinzi iliwabeba Katibu wa CCM Mkoa wa Mwanza Alhaji Mwangi Kundya, Katibu wa CCM Uenezi, Mkoa wa Mwanza, John Mangelepa, Mbunge wa CCM, Viti Maalumu, Maria Hewa na wengineo.
Akizungumzia ajali hiyo ya MV Mlinzi, Alhaji Kundya alisema hakuweza kuamini jinsi ilivyotokea kwani walijikuta wakiwa majini. Walilazimika kuvua viatu na kuacha fedha zao zizame ili waweze kujinusuru, na wala hawakutarajia kuokolewa, lakini muujiza ulitokea na kujikuta wakiokolewa na wavuvi. Ingawa baadaye pia wavuvi waliowaokoa nao walipata ajali baada ya mtumbwi wao kupinduka siku chache.
Inadaiwa kuwa boti hiyo ya MV Mlinzi ilikuwa imezuiliwa kufanya kazi kutokana na kuwa na matatizo. Sasa haijulikani kuwa nani aliiruhusu ilhali ikiwa mbovu, tena ikiwa imezuiliwa kutofanya safari zozote.
Kuanzia mwaka 1996 ajali ya MV Bukoba na 2001 ajali ya treni, tumekuwa tukishuhudia ajali nyingi za majini na nchi kavu kama ajali ya meli ya MV Nyamageni iliyotokea Aprili 28 mwaka 2006 na kusababisha vifo vya watu 50 ambapo miili 6 ilipatikana nchini Uganda na wengine kutopatikana ikiwa ni pamoja na meli yenyewe.
Ingawa ajali mbaya na ambayo haiwezi kusahaulika katika Ziwa Victoria ni ya MV Bukoba. Nyingine ni ile ya treni huko mkoani Dodoma, lakini tangu kutokea kwa ajali ya MV Bukoba ni miaka 14 sasa.
Pamoja na ajali ya MV Bukoba, ambayo haiwezi kusahaulika Mamlaka za kudhibiti au Kusimamia vyombo vya majini kama vile bandari, SUMATRA na mashirika mengine na hata wananchi wa kawaida bado hatujajifunza chochote. Tungekuwa tumejifunza kuhusu ajali hiyo ajali zingine zingeepukika na tungekuwa tunaziepuka kutokana na kwamba abiria tunapokuta chombo kimejaza kupita kiasi, yatupasa kusubiri kingine.
Hata hawa watu wa bandarini hizi meli, boti na mitumbwi zinapokuwa zinapakia abiria wao huwepo eneo hilo na pia tumekuwa tukishuhudia safari hizo zikiambatana na baadhi ya wafanyakazi wa vyombo vya dola, kwanini wasizuie mrundikano wa watu wengi wanaosafiri katika chombo kimoja.
Kwa mantiki hiyo ni kwamba serikali, mamlaka zinazoshughulika na usafiri wa majini, mashirika yasiyo ya kiserikali ambayo pia yanashughulikia suala hilo pamoja na sisi wananchi wa kawaida, hatujajifunza lolote katika ajali ya MV Bukoba iliyotokea mwaka 1996 ambayo pamoja na kupoteza ndugu zetu wengi, tulilia, tukaomboleza na sasa tumesahau tukio zima la ajali hiyo.
mwisho

10 comments:

  1. Borgata Hotel Casino & Spa | New Jersey, United States
    This 진주 출장안마 brand-new hotel 구미 출장안마 features 50000 square feet of gaming. At Borgata's 천안 출장샵 luxurious hotel rooms and suites, you'll experience every 영천 출장안마 room with 구미 출장마사지 all the action

    ReplyDelete