Popular Posts

Friday, September 9, 2011

Rais Kikwete; tukimaliza siasa za umri zinakuja zipi?

Na Deogratius Temba
Tafakuri ya leo haina lengo la kushambulia rais Jakaya Kikwete, nia ni kutaka kujenga mjadala wakiuchokozi katika jamii kujadili kwa kina juu ya aina ya siasa za Chama cha Mapinduzi(CCM).
Rais Kikwete ni Mwenyekiti wa CCM Taifa, ni kada wa siku nyingi atngu akiwa kijana mdogo, amekulia ndani ya CCm ana amepafanikiwa kufikia kiwango cha juu ya kabisa cha uongozi ndani ya Chama. Anajua namna ya kuendesha siasa na hata namna ya kujenga fitina za kisiasa ili kubomua ngome za mahasimu wake kisiasa.
Bila shaka kwa uelewa wangu, aina ya siasa, kauli, na hata nguvu anayoitumia Mwenyekiti Kikwete, tunazichukulia kuwa zina Baraka za chama na sii za kwake binafsi. Akitukana tutasema CCM imetukana kwasababu yeye ndiye alama(symbol) ya chama popote.
Kwa bahati mbaya, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatamka suala la usawa wa kijinsia na kukataza ubaguzi wa aina yoyote katika kutoa haki mbalimbali hapa nchini. Katiba inamtaka kila mwananchi kuishi kwa amani na kupata haki zote zikiwemo za kisiasa (Kugombea, kuchaguliwa na kuchagua mgombea unayemtaka).
Rais Kikwete anajua namna alivyofanikiwa kucheza karata ya siasa chafu yeye na wasaidizi wake wa kisiasa wakati wote wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, na kufanikisha, ijapokuwa mfumo wa siasa zao ulifanikisha uchaguzi CCM ikashinda na kusababisha hasara kubwa ya mpasuko wa udini kwa Taifa hili. Sijengi hoja hii kwa mrengo wa kipinzani lakini ninakiri kuwa siasa za CCM kwa wakati huu ni siasa za kupenda kuhubiri ukabila, udini, na sasa zimeingia kwenye umri.
Hivi karibuni akiwa mkoani Kigoma, Rais alisikika akimweleza Mbunge wa Kigoma Kaskazini kwa Tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) Zitto Kabwe kuwa vijana wasikubali kumchangua Rais mwenye umri mkubwa kama wakwake (Rais Kikwete). Anatamka kuwa yeye ni mzee na asingependa rais anayemridhi mwaka 2015 awe mzee kama yeye.
Kuna maswali ya kujiuliza; je haya maneno ni kwanini rais Kikwete(Mwenyekiti wa CCM) anayazungumzia Kigoma?, ni kwanini amweleze Zitto? Je Zitto ana mahusiano gani na CCM? Je ni vijana wapi anawalenga wa CCM au wa CHADEMA? Au vijana wake wa CCM wameshagwanyika sasa amekata tama, anataka kuwaachia madaraka vijana wa Chadema?
Pia tujiulize Je Kauli ya Rais Kikwete imetoka ndani ya Chama au ni ya kwake mwenyewe? Je wanachama na viongozi wenzake wanajua mpango huo wa kurasimisha madaraka ya urais kwa vijana?
Suala hili lina utata ndani yake, kuna mambo mawili yamefichika kwa rais Kikwete, labda kuijenga CCM au kuibomoa au kukijenga au kukibomoa Chadema. Binafsi na hata Watanzania wengi wenye mapenzi mema na Taifa hili, hawana haja na kauli za kichama, ila hatutaki kauli za kutugawa, hatutaki wanasiasa wanaotaka kutugawa au kutupandikiza chuki na kuvuruga amani iliyojengwa na hayati Baba wa taifa Mwalimu Julius Nyerere. Tuanataja viongozi wenye nia njema na taifa hili, wenye uchungu na amani yetu ambao wanataka kutuunganisha na sio kutugawa.
Sote tunajua jinsi ambavyo taifa letu linapita katika kipindi kigumu kabisa cha mpasuko wa Kisiasa, siasa chafu za majitaka. Siasa za kikabila na udini ambazo ni makovu ya uchaguzi Mkuu uliopita. Siasa hizi za ukabila zilipandikizwa na CCM kwa wananchi kuwa Chadema ni chama cha kikabila. CCM ilitumia nguvu kubwa kuhalalisha uongo na uzandiki ambao leo hii tusipokuwa makini baada ya miaka michache utaliumiza taifa hili.
Tutakumbuka kuwa muda mfupi kabla ya kampeni za uchaguzi Mkuu hazijaanza hakukuwa na dalili yoyote ya maneno ya udini lakini baada ya kampeni kuanza na baada ya uchaguzi, kuna chuki za kikabila na udini nchini.
Katika suala la Udiini, CCM ilipandikiza kauli za kuwa kuna wagombea wadini, kuna watu wadini, kuwa inataka kukomesha udini nchini wakati inajua kuwa imetawala kwa miaka karibia 50, na kama kungekuwepo na udini unakuwa ni udhaifu wa serikali yao. CCM na Mwenyekiti wakaanza kampeni kali za kuhubiri kuwa kuna udini nchini. Matokeo ya mahubiri ya Rais Kikwete yameonekana baada ya siku chache,uchaguzi umeisha bado kuna mpasuko mkubwa, chuki na mgawanyiko wa udini nchini.
Leo hii kuna kundi la viongozi wa kidini ambalo lilitumika na CCM kuhubiri udini, lilitumia kusambaza nyaraka mbalimbali kushambalia dini nyingine sasa linadai haki ya ajira serikalini. Kwa hili CCM hawawezi kujitoa ni matunda ya kampeni za mwaka 2011. Kundi hili tayari limeshatumia vyombo vyake vya habari kutangaza vita na serikali iliyoko madarakani kuwa itaipeleka mahakamani kwa kuwa imeajiri waumini wa dini nyingine kuliko ya kwao. Haya ndio matunda ya wanasasiasa kuhubiri udini ni matunda ya serikali ya CCM. Huu ni moto ambao umewashwa na CCM kwa kauli zao sasa wasubiri kuungua. Wanapaswa kuuzima la sivyo wataungua wenyewe.
Ndivyo ilivyo kwa kauli hata hizi za umri nakandalika zina madhara makubwa mbeleni. Kauli kama hizi zitakiua chama au kuvuruga amani ya Taifa hili. Zitaongeza migawanyiko, mifarakano na hatmaye tutaingia katika vita vya kidini au kikabila.
Mwenyekiti wa chama na wenzake wakiamua wanaweza kutugawa kwa maneno yao. Rais Kikwete, ameanza siasa za udini zimefanikiwa kutugawa, ameingiza nyingine za umri ukimaliza ataanza zipi? Tukumbuke kuwa Umoja ni nguvu, tukigawanyika tu kikabila,kidini, kiumri tunawapa adui zetu nafasi ya kututeka au kutushambulia.
Tunajua kuwa rais Kikwete anarusha makombora hayo ya umri kwa mahasimu wake kisiasa kama Edward Lowassa ambaye anatajwa kuwa mgombea urais 2015, ambaye kiumri wanakaribiana, lakini kuna haja ya kuangalia madhara kitaifa kuliko kumtizama mtu mmoja na kuligawa taifa.

No comments:

Post a Comment