Popular Posts

Friday, March 26, 2010

KUELEKEA UCHAGUZI MKUU 2010

Kanuni sheria ya uchaguzi kurejeshwa kwa wadau
*wagombea kuwa na waasibu
*utitiri wa wajumbe kwenye kampeni basi
Kanuni za utekelezaji wa sheria ya gharama za uchaguzi iliyoipitishwa na kikao cha 18 cha Bunge, Februari mwaka huu mjini Dodoma na kutiwa sahihi na rais Jakaya Kikiwete, Ikulu hivi karibuni zitafanyiwa marekebisho na kujadiliwa tena na wadau wote baadaye.
Akiwasilisha mapendekezo ya kanuni hizo kwa wadau Msajili wa Vyama vya Siasa, John Billy Tendwa, alisema kwamba mjadala huo uliofanyika kwenye ukumbi wa Karimjee Machi 22, mwaka huu ni hatua ya kwanza ya kuwashirikisha wadau wote.
Aidha, Tendwa alisema kwamba kanuni hizo zimelenga katika kuhakikisha kwamba utekelezaji wa sheria ya fedha za uchaguzi unafanyika katika mazingira ya uelewa na yaliyo sawa kwa vyama vyote.
Kanuni zinaelekeza namna ya kutekeleza sheria iliyokwisha kutungwa na kutiwa sahihi na rais wa nchi.katika hotuba kwa wadau Tendwa alieleza kwa ufupi mambo yaliyopo katika kanuni hizo.
Ili kuweka uwazi katika gharama za uchaguzi kanuni zimeeleza kuwa wagombea watatakiwa kuwa na wataalamu wa mahesabu kwa ajili ya kuandaa na kuweka kumbukumbu ya matumizi ya takayofanyika kama gharama za uchaguzi.
Kwa mujibu wa kifungu cha 15(1) cha kanuni za sheria ya gharama za uchaguzi iliyopitishwa na Bunge katika mkutano wa 18 wa Bunge mjini Dodoma Februari mwaka huu na kutiwa sahihi na rais Jakaya Kikwete wiki iliyopita, kila mgombea wa chama cha siasa atapaswa kuwa na mtaalamu wa hesabu ambaye ataweka kumbukumbu za matumizi yake ya kampeni.
“….Mgombea wa chama cha siasa au kikundi ambacho kitahusika katika kanuni hizi, atatakiwa kuwa na mtaalamu wa mahesabu(Accountancy) na ukaguzi kwa ajili ya kuandaa na kuweka kumbukumbu ya matumizi yaliyofanyika kama gharama za uchaguzi” imeeleza sehemu ya kanuni hiyo.
Katika mjadala wa wazi uliowashirikisha wadau wa uchaguzi ulioandaliwa na ofisi ya Msajili wa Vyama Vya siasa na kuhudhuriwa na wawakilishi wa asasi za kijamii na vyama vyote vya siasa wadau walipata nafasi ya kuchangia na kukosoa pale walipoona panafaa kufanya hivyo.
Katika mjadaja huo, msajili wa Vyama John Tendwa aliweka bayana kuwa ofisi yake itayapokea mapendekezo ya wadau hao.
Kanuni zimeeleza kuwa katika kumbukumbu za fedha ambazo mhasibu huyo atapaswa kuzitunza ni kiasi ambacho mgombea au chama cha siasa kilikuwa nacho awali, kiasi alichopata mgombea ua chama baada ya taarifa ya uwazi wa mapato na matumizi kwaajili ya michango na kiasi ambacho kikundi au chama kilitumia kwaajili ya elimu au ushauri kwa umma.
Sehemu hiyo ya nne ya kanuni hizo, imeonyesha utaratibu wa marejesho (Procedure for Making returns) katika kifungu cha 14(1), na kueleza kuwa mgombea atatayarisha taarifa inayohusu marejesho ya matumizi aliyoyafanya wakati wa kampeni za uchaguzi na uchaguzi wenyewe.
Taarifa inayohitajika itatakiwa kuonyesha mahesabu ya matumzi yaliyofanyika, mahesabu ya fedha alizopata mgombea, billi pamoja na stakabadhi, kiasi cha fedha kilichogawiwa na chama cha siasa na ripoti ya mkaguzi wa mahesabu.
Pia kanuni hizo imeweka idadi maalumu ya timu ya kampeni itakayotembea na wagombea kuanzia siku ya kwanza hadi ya mwisho.
Tofauti na chaguzi zilizopita hapa nchini mabadiliko haya yaliyoko katika kanuni hizi yanawataka wagombea kutuma majina ya timu ya wajumbe wa kampeni katika mamlaka na sheria ya gharama za uchaguzi chini ya kifungu kidogo cha tatu na cha saba cha sheria hiyo.

“…Wajumbe watakaounda timu ya kampeni kwa mujibu wa kanuni 16(1) ni …. Kwa mgombea urais wajumbe hawatazidi 50, Ubunge 20,Udiwani 10.Majina ya wajumbe hao yatawasilishwa kwenye mamlaka husika siku 10 kabla ya uteuzi au siku 10, baada ya uteuzi wa wagombea,”

Pia imeeleza kuwa mgombea yoyote atakayetaka kubadilisha timu yake ya kampeni wakati zoezi likiendelea atapaswa kwenye mamlaka inayohusika kwaajili ya mabadiliko hayo.
Kanuni hizo zimeeleza kuwa mamlaka hiyo inaweza kukataa kufanyika kwa mabadiliko au kumuondoa mjumbe yoyote katika orodha kama itaridhika kuwa mjumbe huyo anaweza akaadhiri kampeni za uchaguzi.
Katika kusisitiza ukomo wa idadi ya watu wanaondamana na wagombea, kanuni ya 17(1) imekataza kwa mgombea kuimweka mtu mwingine ambaye sii mgombea au mjumbe wa timu kumnadi mgombea kwa wapiga kura.
“Ni kosa kwa mgombea yoyote au mjumbe wa timu ya kampeni kumweka mtu mwingine yoyote ambaye si mgombea au mjumbe wa timu ya kampeni kushiriki katika kumnadi mgombea kwa wapiga kura,”inaeleza

Kanuni ndogo ya (1) iliyotajwa hapo juu haitahusika kwa mgombea urais wakati anamnadi mgombea wa chama chake kwa wapiga kura.
Pia haitahusika kwa mgombea ubunge anapomnadi mgombea wa chama chake kwa wapiga kura, Mwenyekiti au rais wa chama cha siasa katika ngazi ya kitaifa au Katibu Mkuu wa chama cha siasa husika.
Mwandishi Mkuu wa Sheria kutoka ofisi ya mwanasheria mkuu wa Serikali, Casmir Kyuki, alisema katika mjadala huo kuwa makosa yanayoelezwa katika kanuni hizi ni yuale yaliyoko katika sheria husika.
“Sheria hii ambayo imesainiwa na rais imeeleza kila kitu waziwazi, kama mgombea ameonekana ana matatizo chama hakitapoteza nafasi ya kumsimamisha mgombea, bali kitapewa nafasi ya kumsimamisha mtu mwingine. Kama tutamsimamisha mtu siku ya uteuzi wa wagombea msajili anauwezo wa kukata rufaa, hatutaki kosa la mtu mmoja liwe la chama,”alisema Kyuki.
Mwisho

No comments:

Post a Comment