Popular Posts

Friday, March 26, 2010

CCJ kuzinduliwa Jumapili

*sasa wataka wapewe usajili wa kudumu
Na Mwandishi Wetu,
SIKU chache baada ya kutangaza kujizolea zaidi ya wanachama 2000, kutoka mikoa 10 ya Tanzania bara na visiwani, Chama Cha Jamii (CCJ), kinatarajiwa kuzinduliwa rasmi Mach 21.
Pamoja na kuzinduliwa CCJ, kimetangaza kuwa Machi 22, kitakwenda kwa msajili wa vyama vya siasa John Tendwa, kuomba usajili wa kudumu baada ya kutimiza masharti ya kutafuta wanachama 2000.
Akizungumza na Tafakari kwa njia ya simu Mwenyekiti wa muda wa CCJ, Richard Kiyabo, alisema chama hicho kimetimiza masharti yote ambayo yameainishwa kwenye sheria ya vyama vya siasa na kitazinduliwa rasmi siku ya Jumapili Machi 21, mwaka huu.
Alisema Chama hicho kimevuka kiwango cha idadi ya wanachama wanaotakiwa na Msajili wa Vyama vya Siasa kwa ajili ya kupatiwa usajili wa kudumu, baada ya kufanikiwa kupata wanachama 7,000 badala ya wanachama 2,000 waliotakiwa kupatikana katika mikoa 10 ya Tanzania Bara na Zanzibar.
CCJ kimepata mafanikio hayo katika kipindi cha siku 17 tangu kipatiwe cheti cha usajili wa muda Machi 2, mwaka huu.
Kwa mujibu wa sheria ya vyama vya siasa, chama chenye usajili wa muda kinatakiwa ndani ya siku 180 kiwe kimepata wanachama 200 kwa kila mkoa kwa walau mikoa 10 ya Tanzania Bara na Zanzibar, ambapo CCJ ilipewa muda iwe imekamilisha suala hilo hadi Novemba, mwaka huu.
‘Tunatarajia kukizindua chama chetu rasmi siku ya jumapili, katika ofisi nzetu za makao makuu Mwananyamala, maandalizi yamekamilika, na wanachama kutoka mikoa karibu yote watawakilisha wenzao,”alisema Kiyabo.
Aliongeza kuwa baada ya kuzidua chama sherehe ambazo zitapambwa na ngoma na shamrashamra nyingi, na kuhudhuriwa na viongozi wa vyama vingine vya siasa, Jumatatu watakwenda kwa msajili wa vyama vya siasa kuomba usajili wa kudumu.
Akitilia mkazo suala hilo Kiyabo, alisema katika uzinduzi huo, watapokea wanachama wapya, ambao baadhi yao wamewahi kushika madaraka makubwa ndani ya vyama vingi vya siasa.
Pamoja na kusema hivyo Kiyabo, alikanusha kuwepo kwa vigogo kutoka katika Chama cha Mapinduzi(CCM) kwa sasa wanaowasidia na kusema kuwa vigogo wao ni Watanzania zaidi ya milioni 20, ambao hawajajiunga na vyama vya siasa.
‘Tunashangaa watu wanapotuhusisha na vigogo wa CCM, sisi hatuna vigogo kwa sasa, tusubiri watakaorudisha kadi na kukabidhiwa za CCJ ndiyo watakuwa wamejiunga rasmi nasi lakini kwa sasa hatuna vigogo,” alisema Kiyabo na kuongeza:
“Hatubabaishwi na majina yanayotajwa sisi tunajiamini namna ya kukiendesha chama hatuwahitaji vigogo kujiunga nasi. Lakini chaguzi zote tutashiriki,”
Katibu Mkuu wa CCJ, Renatus Muabhi, aliitaja mikoa ambayo chama hicho kimefanikiwa kuvuna wanachama hao kuwa ni Mwanza, Dodoma, Morogoro, Iringa, Mbeya, Shinyanga, Tabora, Pwani, Dar es Salaam na Unguja na Pemba.
mwisho

No comments:

Post a Comment