Popular Posts

Friday, September 9, 2011

TGNP, watetezi wa haki wanaoporwa haki yao kwa miaka 14

Na Deogratius Temba
Ni ajabu na mshangao kuwa kumbe hata watetezi wa haki za kibinadamu wanaweza kuwa wapiganaji kwaajili ya watu wengine lakini wao wakawa waadhirika wakubwa wa kutendewa ukatili na kudhulumiwa haki yao.

Tunapopambana na ukoloni mamboleo na ukatili, wizi na uporaji wa rasilimali za wananchi ni lazima kukemea kwa nguvu zote aina yoyote ya unyonyaji unaofanywa hapa nchini. Hasa pale Watanzania wenzetu wanapogeuka kuwa wanyonyaji. Hili hatulikubali na ndio vita ambayo binafsi katika safu hii nimepigana nayo kwa kipindi kirefu.

Mtandao wa Jinsia Tanzania, umekuwa ukimiliki jengo la ghorofa moja mahali zilipo ofisi za makao makuu Mabibo Dar es salaam- wanahujumiwa na waliokuwa wapangaji kwenye jengo hilo miaka 14 iliyopita. Wapangaji hao sio wa wapangaji wa TGNP lakini wanatumia sehemu ya vyumba kwenye ofisi hiyo kwaajili ya biashara zao tangu mwaka 1997 hadi leo bila kulipa chochote kwa mwenye jengo. Huu ni ukoloni mwingine unaoambatana na unyonyaji, hatuukubali.

Ni jambo la kusikitisha kuona TGNP inawavumilia watu wanaoishi kwenye jengo lao halali kwa kipindi chote hicho bila kulipa kodi ya pango, kodi ya ardhi, kodi ya majengo serikalini, gharama za usafi, umeme, maji, choo na hawana mpango wa kuondoka.

Wapangaji hao wamewapeleka TGNP mahakamani na wameshindwa kesi. Wapangaji wamefanya fujo wiki hii iliyopita , wamewatishia waliotaka kuwaondoa kwa kutumia silaha za jadi kama vile mapanga, shoka, vizu, rungu, fimbo, na wamefikia hatua ya kubomoa hata geti kwa kulikata kwa misumeno ili waweze kuingia katika vyumba ambavyo TGNP ilikuwa imewafukuza. Kwa wiki sasa TGNP hawawezi kutekeleza majukumu yao ya kulijenga taifa hili na kuihudumia jamii kwasababu wapangaji haramu wameng’ang’ania ofisi zao. Je hii ni hujuma inayosukumwa na nani mwenye madaraka?

Wiki hii TGNP ilifanikiwa kutoa mizigo ya baadhi ya wapangaji nje lakini walirudi kwa nguvu siku hiyo hiyo kwa kulazimisha tena wakikata makufuli ya mwenye jengo.

Katika sakata hili ambalo nimekuwa shuhuda, nimeshangaa hata utendaji wa jeshi la polisi hasa kituo cha Polisi Urafiki. Askari wanajua fika kuwa tatizo lipo wapi lakini hawakuwa tayari kutenda haki. Utekelezaji wa amri ya mahakama, unafanyika kwa baraka za mahakama na vibali kutoka sehemu zote husika lakini wanazuia kwa kigezo kuwa ni kuimarisha amani. Lakini ieleweke kuwa haki inayocheleweshwa sio haki lakini ni lazima ipatikane siku moja.

Polisi nawalaumu kuwa ni chanzo cha wavamizi kurudi ndani ya jengo hilo baada ya kutolewa nje Augosti 23,2011, siku ya jumanne bila kuangalia kuwa ni suala linalotekeleza hukumu ya Mahakama Kuu na ya Rufaa.

Sakata hili lilianza je?
Kwa mujibu wa kumbukumbu na nyaraka za kisheria zilizopo, Mtandao wa Jinsia Tanzania ni mmiliki halali wa jengo lenye hati namba 56998, Kiwanja namba 22/3/1 lililoko katika eneo la Mabibo Dar es Salaam.

TGNP, walinunua jengo hilo kutoka kwa Mfilisi (Benki ya Rasilimali Tanzania- TIB) kwa Iliyokuwa ‘Tanzania Sewing Thread Manufacturers Limited’ au kiwanda cha nyuzi, ambayo ilikuwa sehemu ya kampuni tanzu ya Tanzania Textile Company Limited (TEXCO) kwa gharama ya shilingi milioni 200 ambapo makubaliano ya manunuzi yalifanyika Juni 15, 1997.

Serikali au TIB kama mmiliki alifuata taratibu zote za manunuzi kwa kutangaza mchakato wa uuzwaji wa jengo hilo kwenye vyombo vya habari nchini hususan magazeti.

Baadhi ya watumiaji wa ofisi waliokuwa ndani ya jengo hilo wakati TEXCO ikiwa inafilisiwa nao walishiriki katika mchakato wa kununua bila mafanikio ambapo kumbukumbu zinaonesha kuwa waliomba kulinunua kwa gharama y ash. Milioni 100, wakati TGNP walifika milioni 200. Baada ya TGNP kushinda ‘tender’, baadhi ya watumiaji hao, mnano mwezi wa Julai 1997 walifungua kesi namba 215 / 1997 dhidi ya TIB kama mshitakiwa wa kwanza na TGNP mshitakiwa wa pili katika mahakama kuu kupinga maamuzi ya TIB kuiuzia TGNP jengo hilo.

Hukumu ilisemaje?
Kesi hii ilichukua muda mrefu sana takribani miaka kumi na mbili mpaka kufikia tarehe Oktoba 15, 2009, uamuzi wa Mahakama Kuu ulipotolewa na Jaji T.B Mihayo wa Mahakama Kuu hukumu ambayo iliwapa haki TGNP na kuwaamuru walalamikaji kuondoka mara moja na kulipa gharama.

Wakati mchakato wa kutekeleza Hukumu ya Mahakama Kuu ukiendelea, mnano Septemba 19, 2009 walalamikaji walipeleka katika Mahakama ya Rufaa azimio la kusimamisha utekelezaji wa hukumu ya Mahakama Kuu ya kutowatoa kwenye jengo kwa kupitia ombi na 129 la 2009 ombi ambalo limetupiliwa mbali na Mahakama ya Rufaa Agosti 23, 2011.

Ni hatua gani TGNP wanaichukua?
TGNP wamiliki halali wa hili jengo wanapaswa kupewa fursa ya kutekeleza uamuzi wa Mahakama ya Rufaa uliotolewa Agosti 23, 2011, kwa kutumia sheria ya utatuzi wa migogoro ya ardhi ya mwaka 2002, namba 2, ‘The Courts (Land Disputes Settlements) Act, 2002; No.2’ inaruhusu mwenye nyumba anayekubalika kisheria kuchukua nyumba yake kwa kumtoa mpangaji kwa nguvu katika nyumba anayopanga. Sheria hii imeeleza vizuri juu ya mmiliki wa nyumba kumtoa mpangaji asiyefuata taratibu. Jumapili njema napatikana: 0715 686575

No comments:

Post a Comment