Popular Posts

Wednesday, May 26, 2010

Yatima wakatiza masomo kusaka fedha za kutunza bibi zao

*Serikali yaagiza uongozi wa Wilaya ufuatilie
Na Mwandishi Wetu
WANAFUNZI yatima nane ambao ni kati ya 40 wanaosoma shule ya sekondari ya Malama iliyopo kata ya Utengule Usongwe, wilayani Mbeya vijijini, wamelazimika kukatiza masomo na kwenda kufanya vibarua kwa ajili ya kulea wadogo na bibi zao.
Imebainika kuwa hali hiyo imewafanya wanafunzi hao kutokuhudhuria masomo kutokana na kugeuzwa kuwa wakuu wa kaya.
Mkuu wa shule hiyo Mariamu Mwanisenga, ameliambia Tafakari kuwa shule hiyo ina watoto yatima na baadhi yao hali zao za maisha ni mbaya na imekuwa sababu za utoro.
Amesema kutokana na wanafunzi hao nane kuwa wakuu wa kaya inapofika saa sita mchana hulazimika kufika katika ofisi yake kuomba ruhusa kwa lengo la kwenda kufanya vibarua na pesa wanazopata wananunua chakula kwa ajili ya wadogo zao.
“Wanatia huruma sana wanakuja hapa kuomba ruhusa, sasa mimi nalazimika kutoa ingawa si taratibu kufanya hivyo,lakini kutokana na hali zao na majukumu waliyonayo unalazimika kufanya hivyo, maana muda mwingine ukiwakatalia unakuta wanalia sana hadi unaingiwa na uchungu,” amesema Mwalimu Mwanisenga na kuongeza:
“Muda mwingine hukosa pesa na matokeo yake huacha hata kuja shule na ukiwauliza wanakuambia kuwa walishindwa kuhudhuria masomo kwa kuwa wao na wadogo zao walilala njaa na hivyo isingekuwa rahisi kuwaacha katika hali hilyo,” ameongeza.
Amesema hali hiyo imeuweka katika wakati mgumu uongozi wa shule kwa kuwa hulazimika kutumia muda wa ziada kufuwafuatilia wanafunzi hao kwa hofu ya kutojiingiza katika vitendo viovu vinavyoweza kuhatarisha maisha yao.
Aidhaa amesema kutokana na hali hiyo wiki iliyopita aliamua kuitisha kikao cha bodi ya shule ambapo wajumbe wake walikubaliana kugawana wanafunzi hao nane walio katika hali ngumu kwa lengo la kuwanusuru wasikatishe masomo.
Aliwataja wanafunzi hao nane kati ya 40 kuwa ni Janeth Jackson, Yisambi Jackson, Prisca Paul, Benito Kiando wa kidato cha pili, Subira Iddy, Fadhil Mwakyosi Betty Paul wa kidato cha tatu na Alphonce Joseph wa kidato cha kwanza.
Ofisa elimu sekondari wilaya ya Mbeya vijijini Ashiry Komba, amekiri kuwepo kwa tatizo hilo na kueleza kuwa yeye binafsi amechukua jukumu la kuwalea wanafunzi watatu kati ya hao nane wenye hali mbaya zaidi.
“Binafsi nimeguswa hivyo nimeamua kwa makusudi kuwasaidia hao, ingawa hali hiyo imeshafikishwa katika ofisi ya Mkurugenzi ambaye ndiye mmiliki wa shule zote za kata katika halmashauri” alibainisha Komba.
Msemaji wa Wizara ya Jinsia Wanawake na Watoto, Erasto Ching’oro, ameliambia Tafakari, kuwa viongozi wa serikali walioko katika wilaya wanapaswa kufuatalia tatizo hilo na kuwasaidia watoto hao.
“Kwasababu serikali ya wilaya inayomamlaka ya kuhakikisha watoto wanapata haki ya kwenda shule, kama kuna tatizo watoe maelezo na kama kuna upungufu wa rasimali waripoti Wizarani. Kabila ya Wizara kufanya chochote tunahitaji kuona serikali ya wilaya itueleze imechukua hatua gani na wamefikia wapi,”amesema.
Amesema wazee wasio na uwezo wa kujitafutia chakula hawawezi kuwa chanzo cha watoto kutokupata masomo, kwani serikali katika ngazi husika inapaswa kuchukua hatua kwa kuwahudumia wazee hao.
“Kuna serikali za mitaa, kijiji, kata na wilaya wanatakiwa wajiridhishe na ufuatiliaji wa matatizo ya watoto yatima kama haya,”amesema Ching’oro.
Mwisho.

1 comment: