Popular Posts

Monday, February 1, 2010

Hivi ndivyo Gavana Ndullu, alivyopangua hoja za ujenzi wa kasiri lake Naibu Gavana
* Kamati ya Bunge ilijipanga kumhoji ikagwaya
* Baada ya kumaliza wakampongeza, na kukaa kimya

Na Deogratius Temba

BAADA ya kuwepo kwa maswali lukuki toka kwa wananchi na wadau wa uchumi wa nchi juu ya matumizi makubwa ya fedha yaliyotumiwa na uongozi wa Benki Kuu ya Tanzania(BoT), kujenga nyumba mbili za watendaji wakuu gavana na naibu wake zilizogharimu ziadi ya sh. Bilioni 2.5, Gvana Berno Ndullu alijitetea hadharani.

Gavana alitoa ripoti yake ya utetezi Januari 21, mwaka huu, katika ukumbi wa Karimjee, kwa mara ya kwanza tangu kuibuka kwa tuhuma hizo ukiacha taarifa walioiweka kwenye tovuti ya BoT. Gavana alitokea kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma, kwaajili kutoa hesabu za BoT.

Mbele ya wajumbe wa Kamati hiyo na Mwenyekiti wake Zitto Kabwe, Profesa Ndullu alijieleza bila kuacha hata chembe ya data huku akiwapiga vijembe wale waliokuwa wakimuandika kuwa ametumia fedha nyingi katika ujenzi huo.

Katika makala hii tunakuletea sehemu ya taarifa hiyo na mahojiano yake na kamati.

Mwenyekiti wa Kamat (Zitto): Gavana, leo umekuja mbele ya kamati kwajili ya kutoa ripoti ya hesbabu za BoT, lakini kwa sababu hivi karibuni kuna suala liliibuka na linagusa umma, na kamati hii inahusika na mashirika ya umma, tunapenda uieleze kamati nini kilitokea.Tungependa kufahamu hili la nyumba za Gavana.

Gavana Ndullu, Asante!, ila nitapenda katika kutoa taarifa hiyo, huku nikijibu maswali kadhaa hapa.

Tujiulize, Je nyumba hizi ni za benki au ni za viongozi wake?
Je Nyumba hizi zilihitajika? Na mengine…..”

“Sheria ya Benki Kuu ya mwaka 2006, iliagiza Benki kuu iwe na nyumba . Awali Benki Kuu ilikuwa na viongozi wakuu wawili, Gavana na Naibu wake mmoja. Baada ya mabadiliko ya Sheria ya mwaka 2006, Benki Kuu ina viongozi wakuu wanne; Gavana na Manaibu wake watatu. Kila mmoja wao, kwa mikataba iliyowekwa anastahili kupata nyumba ya kuishi.


Pili, kabla ya hapo Benki Kuu ilifanya uamuzi wa kujenga nyumba mbili zaidi kwa makazi ya viongozi walioongezeka. Iliamuliwa nyumba hizi zijengwe kiwanja namba 57 Barabara ya Mtwara Crescent. na kiwanja namba 12 Barabara ya Tumbawe maeneo ya Oysterbay.

Mwaka 2007, Benki Kuu ikawa imeshampata mshauri mwelekezi, baada ya zabuni kutangazwa mwaka 2007. alipopatikana utaratibu ukaanza wa kuchora ambapo ulichukua miezi mitatu.

Hizi nyumba zilikuwa mbili, ya Gavana na Naibu kwa sababu Naibu mmoja alichukua nyumba iliyokuwa ya Gavana wa zamani, marehemu Daud Balali, mimi nilipoteuliwa na kujiunga na BoT Septemba 2007, niliendelea kuishi kwenye nyumba yangu binafsi iliyoko Mbezi Beach, lakini baadaye nililazimika kuhamishiwa katika nyumba nyingine ya kupanga iliyoko Masaki baada ya kuona ninachelewa kazini kutokana na foleni.

Na pia uamuzi wa kujenga umezingatia pia gharama za kupanga nyumba kwani nyumba niliyokuwa nikiishi Masaki ilikuwa ikilipiwa kodi ya dola 7,000 kwa mwezi.

Zitto akadakia: “ dola ngapi? Ndulu, Elfu saba!

Zitto: kwahiyo tufanye ni sawa na dola 84,000 kwa mwaka?
Gavana Ndukllu: Ndiyo,

Zitto: Kodi ya nyumba uliyokuwa unaishi ya kupanga ni sawa na kujenga nyumba nyingine?

Gavana: kabisa! uamuzi ulifanywa kwa kuliangalia hilo.

Gavana: Nizungumzie utaratibu uliofuatwa, mchakato wa ujenzi ulianza Februari 2008, zabuni ilitangazwa wakajitokeza wazabuni 12, 10 wakarejesha kwa wakati, Aliyekuwa na gharama ya chini alisema ujenzi ungegharimu sh 1,399,184,549 na yule wa juu ni sh 1,847,000,000. Hapo bodi ya zabuni ilikaa ikamteua mwenye gharama za chini.

“Baada ya negotiation (makubaliano) kati ya mzabuni na bodi wakakubaliana kuwa ujenzi wa nyumba moja yaani ile ya gavana ni sh bilioni 1.274 hapo waliingia mkataba wa bei isiyobadilika.

Tulifuata taratibu zote za sheria ya manunuzi ya (PPRA), nyumba hizi zinatofautina kwa gharama y a sh. Milioni mbili tu, lakini zote ni sawa na gavana au Naibu wake anaweza kuishi moja wapo bila kuichagua. Sisi BoT hatuna nyumba maalumu ya Gavana wote tuko sawa.

Gavana: Wameandika sana ila Mimi ni Mndamba safi, nimeanza kuogelea nikiwa na miaka mitatu...sihitaji swimming pool. Nimezaliwa kijijini, nimeogelea sana kwenye mito, hata ikiondolewa sitakosa kitu.

Anaendelea kusema: Nyumba zote nilizowahi kuishi hazina swimming pool hata ile niliyojenga mwenyewe ya Mbezi haina bwawa la kuogelea.

WakatiGavana Ndullu akieleza hayo wabunge wa kamati hiyo walikuwa wakimsikiliza kwa makini, huku utulivu ukiwa umetanda kwenye chumba hicho kilichokuwa kimefurika wanahabari.

Gavana aliendelea: Napenda kuweka wazi, ulinzi kwa gavana ni kitu muhimu sana. Leo nikitekwa mimi si jambo dogo…ndiyo maana ujenzi wa nyumba hizi ulizingatia sana ulinzi. Kwa wanaolifahamu eneo hili upande mmoja kuna ukuta mrefu wenye usalama.

Kwa zaidi ya dakika 35 gavana huyo alikuwa akiieleza kamati hiyo ya Bunge chanzo na mchakato mzima wa matumizi ya fedha hizo, huku akisisitiza kwamba nyumba hizo ni mali ya BoT kwa ajili ya gavana yeyote atakayekuja, kabla ya kutaja gharama za bwawa la kuogelea kuwa ni sh milioni 40.


Zitto: Gavana, unaweza kutumbia nyumba hizi zitajilipa baada ya muda gani?

Gavana: Zitaanza kujilipa baada ya miaka 12.

Zitto: zitadumu muda gani? Gavana: baada ya miaka 100.

Baada ya Kuhitimisha taarifa hiyo, Gavana alisema amemaliza na Mwenyekiti Zitto, aliwataka wabunge waulize mwaswali.

Kwa muda kulikuwa na ukimya huku wabunge wakivuta subra.

Mwenyekiti Zitto, Mhe. Diallo!

Antony Diallo: Kwanza nimpongeze Gavana kwa jinsi alivyotumia akili kupunguza ghrama unajua huko Ostabay huwezi kupata kiwanja cha chini y ash. milioni 500, hapo wao walijitahidi sana.

Peter Serukamba: Gharama ulizozitaja hapo ni pamoja na za kuchora au ni tofauti?

Gavana: hizo hazipo zilifanyika awali

Zitto: wabunge mmeridhika?

Serukamba: samani za ndani zilinunuliwa wapi?

Gavana: zaidi ya nusu ya samani za ndani ni zangu nilizohama nazo na chache zilinunuliwa.

Esterina Kilasi: Gavana fedha zote ulizotenga kwajili ya ujenzi huo zimetumika? Gavana: hapana, hadi sasa hazijafikia kiasi hicho.

Zitto: Sawa Gavana tumekusikia suala hili litatokea kwenye hesabu za BoT za Juni mwaka huu. Tunamwomba CAG akague suala hesabu hizo.

Zitto ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini(Chadema), aliendeleza pongezi kwa gavana na kubainisha kwamba hesabu na gharama za ujenzi huo zitapitiwa na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa lengo la kukutana nazo kwenye hesabu zinazoishia Juni mwaka huu.
0784/715 686575
www.deotemba.blogspot.com
mwisho

No comments:

Post a Comment