Popular Posts

Thursday, January 28, 2010

Naiona Tanzania mpya ikizaliwa baada ya miaka 10

MAANDIKO matakatifu yanasema kuwa ipo siku Mbingu zitageuka na nchi itaumbwa upya. Hayo ni maneno ambayo kwa kila anayeamini mabadiliko atajua kuwa kuna kila jambo lina siku yake na kila lenye mwanzo lina mwisho wake.

Binadamu amekuwepo duniani na muda wake ukimalizika anaondoka. Ndivyo ilivyo kwa vitu vyote vilivyoumbwa. Katika imani ipo siku nao ulimwengu utabadilika, na kuumbwa upya nyota, mwezi na jua vyote vitatoweka na kuwepo kwa aina nyingine ya mbingu.

Kwa hali ilivyo, Tanzania inaweza kubadilika kwa kiasi kikubwa na kuwa nchi mpya. Kwa Tanzania tayari ninaiona Tanzania mpya ikizaliwa baada ya miaka 10, au chini ya hapo. Baada ya kupitia katika kipindi kigumu chenye changamoto kubwa kwa kipindi cha miaka zaidi ya 10 sasa ambayo taifa limekuwa bila ya Marehemu Baba wa Taifa, hakika taifa linaweza kuzaliwa upya.

Zipo ndoto zilizootwa na wazee wetu, kuwa ipo siku mambo yatabadilika, hayati Baba wa taifa naye aliiota, alisema ipo siku hata CCM itameguka na kuzaliwa kwa chama kipya cha upinzania chenye nguvu. Likitokea hilo Tanzania mpya itakuwa imezaliwa.

Rushwa , ufisadi, unyanyasaji na ukiukwaji wa haki za binadamu unaofanywa hautakuwepo tena kwani viongozi tulionao watakuwa wamekwisha!

Ni kweli ipo siku Tanzania itazaliwa upya na viongozi wa kuliongoza taifa watazaliwa pia. mbingu zitakuwa zimegeuka na nchi imeumbwa upya, ndiko tunakoelekea sasa.

Taarifa za wiki hii kuwa kuna chama kipya kinaitwa Chama cha Jamii (CCJ), ambacho kwa ndoto na maono ya watu wengi kuna uwezekano mkubwa watu wanaolitakalia taifa hili mema wakajiunga na kuleta mabadiliko makuwa, inaweza kuwa mwanzo wa nchi kugeuka na kuumbwa upya.

Mwandishi Ayi Kwei Armah kutoka Ghana katika kitabu chake cha ‘The Beautiful Ones Are Not Yet Born’ (1969)
aliandika kuhusu tatizo sugu la uchafu wa kifisadi ulioikumba Ghana baada ya uhuru katikati ya miaka ya ’60.

Mwanazuoni Armah ameeleza kwa kina na kuonyesha jinsi Ghana ilivyooza kwa rushwa baada ya uhuru chini ya utawala wa Rais Kwame Nkrumah, mwaasisi wa taifa la Ghana iliyojipatia uhuru wake 1957 kama nchi ya kwanza kupata uhuru barani Afrika.

Wakati huo nchini Ghana, rushwa ilikuwa imekubaliwa katika jamii ya Waghana kiasi kwamba waliokwepa kutoa au kuipokea walikuwa wakionekana kuwa wajinga, wapumbavu na waoga na waliojihusisha na ufisadi; waliopenda kuitoa na kuipokea rushwa walionekana kuwa jasiri na wenye heshima kubwa mbele ya jamii nzima!

Rushwa ikawa njia halali ya kujitajirisha. Ikafanywa kuwa biashara ya kimya kimya iliyofanywa na mawaziri na maofisa wengine wa serikali ya Nkrumah. Viongozi wakaamua kwa ujasiri kuitumia kodi ya wananchi kwa maslahi na manufaa yao binafsi na ya familia na ndugu zao kama vile kununua mashangingi yaliyogharimu mabilioni ya fedha na kujenga nyumba za kifahari.

Hata viongozi wa ngazi za chini wa serikali wakawa huru kutoa na kupokea rushwa. Hata wahasibu wa shule mbali mbali wakaanza kuzitumia pesa za wanafunzi kwa maendeleo yao binafsi.

Watu wote wa tabaka la chini wakakata hata tamaa ya maisha na kutokana na ujinga na woga hawakujua la kufanya. Hata wale waliosoma na kutambulika kama wanazuoni kwa mfano walimu wakaingiwa na imani kuwa matatizo yanaweza tu kutatuliwa kwa ama kuyakimbia au kutokujihusiaha au kujihangaisha nayo! Imani hiyo inapingana na falsafa inayosema kuwa matatizo hayawezi kutatuliwa kwa kuyakimbia.

Kutokana na ugumu wa maisha uliochangiwa na ukithiri na ushamiri wa rushwa iliyokuwa ikiendeshwa na kukuzwa na viongozi na wafanyabiashara, watu wengi wa tabaka la chini wakazikimbia familia zao. Wanawake na wasichana wakaamua kujiingiza katika biashara ya ukahaba na wengine katika utumiaji wa madawa ya kulevya kwa imani kuwa wangeyasahau masumbuko na taabu za maisha yao.

Wale watu katika jamii ya Waghana ambao walionekana kuchukia rushwa wakati huo wakafananishwa na ndege aitwaye ‘Chichidodo’ ambaye hupenda sana kula buu au funza lakini huchukia sana kinyesi ambacho ndicho chanzo cha funza. Hii ilikuwa na maana kuwa hata wale waliojifanya kuchukia rushwa walikuwa wakipenda kupata au kutumia vitu vitokanavyo na vitendo vya rushwa.

Mwishowe ikafikia mahali Waghana wakachoka na vitendo vya rushwa vilivyokuwa vikifanywa na watawala wao baada ya hali yao ya maisha kuwa ngumu zaidi. Jeshi likafanya mapinduzi ya kuung’oa utawala wa Rais Nkrumah.

Ndio maana hata leo wengi wanalalamika na kunung’unika juu ya jamii hovyo yenye matabaka, uongozi mbaya, ushirikiana, udikteta, ukosefu wa demokrasia, unyonyaji, unyanyasaji, uonevu, udunishaji na udhalilishaji wa wanawake katika jamii, rushwa au ufisadi, uvunjaji wa haki za binadamu n.k

Viongozi na matajiri walichokijali ni pesa na utajiri kuliko utu wa wengine huku wananchi wa kawaida wakitaabika na kuteseka kwa machungu ya ugumu na ughali wa maisha yao ambao ulichangiwa na rushwa, uzembe na usaliti wa viongozi na unyonyaji uliofanywa dhidi yao (wananchi) viongozi kwa kushirikiana na matajiri.

Ujio wa CCJ unaweza kuondoa hadha hii na kuifanya Tanzania kuwa mahali salama pa kuishi. Kutokuwepo kwa CCM madarakani labda inaweza kuwa mwanzo wa kurejea kwa neema ya ukombozi Tanzania.

Utumwa ambao watanznaia wamekumbana nao kwa takribani miaka 48 ya uhuru wakiishi katika taifa la wajanja wala rushwa, huku rushwa ikikomaa na kubadilishwa majina kila mara, linaweza kufikia mwisho wake.

Lakiani yote haya yapo mikononi mwa watanznaia wenyewe ndiyo wenye uwezo wa kuamua ama kuiacha Tanzania ibaki kuwa kama ilivyo au izaliwe upya kwa kufanya mabadiliko na kuyakubali.

Tutaonana wiki ijayo

0784/715 686575
deojkt@yahoo.com
www.deotemba.blogspot.com

No comments:

Post a Comment