Popular Posts

Tuesday, October 20, 2009

Serikali kutoa taarifa ya Richmond mbele ya Bunge leo

*Hatma ya Mwanyika,Dk. Hoseah na Madata leo
*Kamati: lisipomalizika leo tuulizwe sisi



SERIKALI inayatarajiwa kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa maazimio 21 ya Bunge juu ya kampuni ya kufufua umeme wa dharura ya Richmond Development LLC, inayodaiwa kupewa zabuni kinyume na taratibu.

Taarifa hiyo ya serikali itatolewa leo mbele ya kamati ya kudumu ya Bunge ya Madini na Nishati, na Waziri wa Nishati na Madini Wiliam Ngeleja.

Kwa mujibu wa ratiba ya vikao vya kamati hiyo, ambayo wiki iliyopita ililazimika kubadilishwa kutokana na Waziri Ngeleja kutokuwepo, imeonyesha kuwa leo kamati hiyo itapokea taarifa hiyo na kuijadili ikiwa ni pamoja na kuangalia kama inajibu maswali na maagizo ambayo wabunge waliipa serikali wakati wa mkutano wa 16 wa Bunge.

Taarifa ya kwanza ya utekelezaji iliwasilishwa Bungeni Julai 25 mwaka huu ambapo ilikataliwa na serikali kutakiwa kuwawajibisha baadhi ya watendaji wa serikali ambao walihusika kwa uzembe ambao ulilisababishia taifa hasara.

Mwenyekiti wa kamati hiyo, Wiliam Shelukindo, alisema Bunge linatarajia serikali itajibu maswali yote ambayo yameulizwa na wabunge ikiwa ni pamoja na kuwawajibisha wale waliotakiwa kuwajibishwa.

Alisema pia serikali inatakiwa kuelewa kuwa umefika wakati suala hilo la Richmond limalizike kwani limechukua muda mrefu.

Shelukindo alisema kama ripoti hiyo ya serikali itakayo wasilishwa leo haitaonyesha kulimaliza suala hilo yeye na kamati yake waulizwe.

Baada ya kamati hiyo kupokea taarifa kutoka serikalini leo itajadiliwa kwa siku mbili na wajumbe wa kamati hiyo, ambapo kama itawaridhisha wataruhusu serikali kuiwasilisha Bungeni Katika mkutano wa 17 unaotarajiwa kuanza Jumanne ijayo Oktoba 27, mwaka huu.

Katika mkutano wa 16, wa Bunge serikali iliwasilisha ripoti ambayo ilieleza kuonywa kwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(Takukuru), Edward Hoseah kutokana na kutokuwa na umakini wa kutosha wakati taasisi yake ilipofanya uchunguzi wa mchakato wa mkataba huo.

Pamoja na Hosea mwingine aliyeonywa ni aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Majadiliano ya Wataalam, Singi Madata.

Katika ripoti hiyo iliyosomwa na Naibu Waziri wa Nishati na madini Adam Malima, kwa niaba ya serikali, ilieleza kuwa Hosea alionywa kutokana na mamlaka yake ya nidhamu kuona kuwa sheria ya Takukuru kwa wakati huo ilikuwa na mapungufu katika kubaini viashiria vya rushwa kwenye mchakato wa zabuni ambavyo ndiyo wataalamu wa Takukuru walijikita kufanya uchunguzi wao.

Kwa mujibu wa serikali taarifa ya Hosea haikuonyesha bayana tofauti baina ya Makampuni ya Richmond Development Company(LLC), RDEVO na Richmond Development Company(RDC) jambo ambalo lilijitokeza baadaye wakati Kamati Teule ya bunge ilipofanya uchunguzi wake.

Kuhusu Madata, serikali ilisema katika utetezi wake, Mamlaka yake imeona kuwa kwa mujibu wa maelekezo ya kazi waliyopewa ya kusaili makampuni nane yalioomba zabuni ya kufua umeme wa dharura alieleza kuwa kazi hiyo ilifanyika kwa muda wa siku mbili.

Serikali ilisema hapakuonekana dalili za mazingira ya rushwa wakati wa kufanya kazi hiyo hivyo mamlaka yake ya nidhamu ilitoa onyo kwa Madata kwa kutokuwa mwangalifu katika eneo hilo

Kuhusu Mwanasheria Mkuu wa serikali ambaye Mamlaka yake ya nidhamu ni Rais, taarifa hiyo ilieleza kuwa maelezo walionayo ni kuwa hakuna kosa lolote la kisheria au kinidhamu ambalo alilifanya katika nafasi yake kama Mwanasheria Mkuu wa serikali katika mchakato mzima ulioipa ushindi kampuni ya Richmond Development Company, LLC katika zabuni ya kuzalisha umeme wa dharura

Kwa mujibu wa ripoti hiyo iliyozua mjadala mkubwa na kupingwa na Wabunge wengi, kwa ujumla ilionyesha kuwa uchunguzi wa vyombo vya dola kuhusu watumishi wote wa umma waliohusika na suala hili, unaonyesha kuwa hakuna mtumishi yeyote aliyeonekana kutenda kosa la jinai lenye kuhitaji kuchukuliwa hatua za kisheria

Katika maazimio ya bunge yaliitaka serikali kuwawajibisha watumishi wote wa umma waliohusika katika madajiliano ya mchakato mzima wa mkataba wa baina ya Tanesco na Richmond pamoja na wa Takukuru waliofanya uchunguzi wa suala hilo .

Kuhusu watumishi wa umma waliohusika katika majadiliano ya mchakato mzima wa makataba huo, serikali imewawajibisha watendaji wake wakiwemo maofisa waandamizi ambao ni aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Uchumi, Gray Mgonja, Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, walifunguliwa mashtaka ya nidhamu kwa mujibu wa kanuni namna 49(1) ya sheria ya utumishi wa umma ya mwaka 2002.

Kuhusu azimio namba nane na 14 ya bunge kutaka serikali kuwawajibisha viongozi wenye dhamana ya kisiasa waliokuwa Mawaziri wa Wizara ya Nishati na Madini, Dk. Ibrahim Msabaha na Nazir Karamagi, taarifa hiyo ilisema kama ilivyoelezwa katika mkutano wa 18 wa bunge kwamba vyombo vya dola vimekuwa vinaendelea na uchunguzi wake kuhusu suala hilo hadi sasa suala hilo halijafikia tamati kwa kuwa linashughulikiwa zaidi na taasisi ya Takukuru pamoja na ofisi ya Mkurugenzi wa Mashkata Nchini, DPP.

Kwa mujibu wa serikali kuhusu azimio la bunge kutaka wamiliki wa Richmond LLC na Richmond Development Company(T) ltd, walifunguliwa kesi ya jinai mara moja kwa udanganyifu na ujanja wa serikali, ilieleza kuwa iliunda kamati maalumu ya vyombo vya dola ili kushughulikia uchunguzi na upelelezi kuhusiana na maazimio hayo mawili.

Wakati Bunge likitaka watu zaidi waliohusika wawajibishwe tayari mmoja wa wawakilishi wa kampuni ya Richmond, Naeem Adam Gire, ameshafikishwa katika mahakama ya Kisutu, Dar es Salaam Januari 13 mwaka huu na kusomewa mashtaka matano ya makosa ya jinai.
Mwisho

3 comments: